Tarehe : Nov. 25, 2019, 7:58 a.m.
Na Asteria Muhozya, Dodoma
Benki ya NMB imeshauriwa kutumia fursa za Kibiashara zilizopo katika Sekta ya Madini zikiwalenga Wachimbaji Wadogo na wa Kati wanaofanya shughuli hizo katika sekta husika ikiwemo kujifunza namna biashara ya Madini inavyofanyika.
Rai hiyo imetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Prof. Simon Msanjila wakati wa kikao baina yake na Ujumbe wa Wataalam kutoka Benki hiyo ulioongozwa na Mkuu wa Idara ya Mahusiano ya Serikali ya Benki hiyo, Vicky Bishubo. Kikao hicho kimefanyika Novemba 25, 2019, jijini Dodoma.
Aidha, kauli ya Katibu Mkuu kwa benki hiyo inafuatia juhudi za Serikali kupitia Wizara ya Madini zinazolenga katika kuwapatia elimu Wachimbaji ikiwemo za kutunza kumbukumbu za uzalishaji, kufanya tafiti ili kujua kiasi cha mashapo kupitia Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST), na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), hayo yote yakilenga katika kuwawezesha wachimbaji hao kukopesheka na Taasisi za Fedha.
Pia, Prof. Msanjila ameitaka benki hiyo kutumia fursa zilizopo katika masoko ya Madini yaliyoanzishwa katika mikoa mbalimbali nchini ili kurahisisha biashara ya Madini na kutolea mfano wa Soko la Madini Arusha kwamba benki hiyo haina huduma katika soko hilo huku biashara ya Madini sokoni hapo ikifanyika kwa kiasi kikubwa.
Aidha, Prof. Msanjila ameitoa wasiwasi benki hiyo kuwa, hivi sasa biashara za Madini zinafanyika katika mfumo ulio wazi tofauti na ilivyokuwa awali na kuongeza kwamba, “kuna biashara nyingi kwenye sekta ya madini. Niwaambie hivi karibuni Serikali ya Qatar itaanza kununua dhahabu moja kwa moja kutoka Geita.”
Katika hatua nyingine, kama ilivyoainishwa katika Ibara ya 35(j) ya Ilani ya Uchaguzi wa Chama Cha Mapinduzi ya Mwaka 2015-2020 kuhusu Kusimamia na kuhamasisha uwekezaji katika shughuli za uongezaji thamani madini ili kukuza mchango wa sekta hiyo katika Pato la Taifa, Prof. Msanjila ameishauri benki hiyo kuangalia namna ya kufanya biashara katika tasnia ya ukataji wa madini, akieleza kwamba, ni miongoni mwa masuala yanayopewa kipaumbele na serikali ya kuhakikisha madini yanaongezwa thamani kabla ya kusafirishwa nje ya nchi.
“Sekta ya madini haijatumiwa vizuri na mabenki ninawakaribisha kwenye sekta hii . Pale Arusha ndo mji pekee wa Ukataji Madini ya Vito. Mwende mkaliangalie hili,” amesisitiza Prof. Msanjila.
Naye, Mkuu wa Idara ya Mahusiano ya Serikali ya Benki hiyo, Vicky Bishubo amemshukuru Prof. Msanjila kwa kueleza fursa zilizopo katika sekta husika na kueleza kwamba, benki hiyo imeyachukua kwa uzito mkubwa yote yaliyoelezwa na iko tayari kuyafanyia kazi.
“Tumejifunza namna sekta ya Madini inavyofanya kazi kuna uwezekano wa sisi kuandaa mfumo wa kuwasaidia wachimbaji wadogo,” ameeleza Bishubo.
by: madini
Waziri wa Madini, Doto Biteko ameyataka Mabenki ya ndani kushirikiana ili kuweza kuzikopesha kampun…
by: madini on: April 23, 2021, 5:11 a.m.
Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula amesema kuwa katika kipindi cha mwezi Julai, 202…
by: madini on: April 28, 2021, 12:51 p.m.
’Nimeona Nyuso Zenye Furaha , Amani na Utulivu’’ Ninayo furaha kuwa nanyi hapa ili tuanze safari hi…
by: madini on: Jan. 10, 2022, 2:55 p.m.
Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa ameiagiza Tume ya Madini kutafuta Masoko ya wanunuzi wa…
by: madini on: Jan. 30, 2022, 9:32 a.m.