Tarehe : May 24, 2018, 11 a.m.
Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko amemwagiza Kamishna Msaidizi wa Madini Kanda ya Kaskazini, Adam Juma kumwondoa Kaimu Afisa Madini Mkazi wa Mererani, Fredrick Girenga kwenye wadhifa huo na kumweka Afisa mwingine atakayemudu vema usimamizi wa Ukuta wa Mererani unaozunguka machimbo ya Tanzanite.
Kiberenge maalum kinachobeba watu na malighafi yenye madini ya tanzanite, kikipita katika njia yake kushuka chini shimoni kunakochimbwa madini hayo, kama kilivyokutwa katika Mgodi wa Franone uliopo Kitalu D Mererani, wakati wa ziara ya Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko, Mei 23 mwaka huu.
Biteko alitoa agizo hilo jana, Mei 23, baada ya kufanya ziara kukagua shughuli zinazoendelea Mererani, hususan kwenye Ukuta na kubaini udhaifu katika uchukuaji na utunzaji wa kumbukumbu za wahusika wanaoingia ndani ya eneo hilo na kutoka, pamoja na mali (madini) yanayotolewa kupitia getini.
“Mheshimiwa Rais amewekeza pesa nyingi sana hapa. Haiwezekani sisi watendaji tushindwe kujituma hata kwa mambo madogo kama haya ya kusimamia vema utekelezaji wa ulinzi wa rasilimali hizi; yaani tusubiri yeye aje tena mwenyewe kutuelekeza hata mbinu ndogo za udhibiti. Lazima tuwe wabunifu na wenye kujituma,” alisisitiza.
Alisema kwamba, yeyote atakayepangwa kufanya kazi ya usimamizi wa Ukuta huo ajue kwamba macho la Serikali yameelekezwa mahali hapo. “Hata usipomwona Waziri, Naibu Mawaziri, Katibu Mkuu na Kamishna wa Madini, ujue macho yetu yapo huku na usipotimiza wajibu wako kwa kiwango kinachoridhisha tutakuwajibisha mara moja.”
Akizungumza na waandishi wa habari, baada ya kuhitimisha ziara yake, Naibu Waziri alifafanua kuwa, udhaifu ulioonekana ni kwa upande wa Wizara ambapo alitoa mfano kuwa; hakuna rekodi yoyote inayoonesha nani anaingia, kwa muda gani, na nani amepangwa kufanya kazi ipi. Aliongeza kuwa, hata rekodi ya namna mzigo unavyotoka ndani kwenda nje ya migodi kupitia getini, haipo.
Kuhusu maelekezo aliyoyatoa ya kubadilishwa kwa Afisa Madini Mkazi anayesimamia eneo hilo; Biteko alifafanua kuwa, Wizara haiwezi kuruhusu mtu yeyote kuirudisha kwenye udhaifu wa usimamizi thabiti wa rasilimali za madini, hususan baada ya jitihada kubwa zilizofanywa kuisaidia sekta ya madini iweze kukua.
Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko (wa pili kulia), akimsikiliza Kaimu Afisa Madini Mkazi wa Mererani, Fredrick Girenga (katikati) kuhusu utaratibu unaotumika kuweka kumbukumbu za watu na mali/madini wanaoingia na kutoka katika migodi ya tanzanite. Hapo ni katika Lango/Geti la kuingilia na kutokea kwenye eneo la migodi hiyo lililozungushiwa Ukuta hivi karibuni kwa amri ya Rais John Magufuli. Naibu Waziri alikuwa katika ziara ya kazi Mererani, Mei 23 mwaka huu.
“Kusema kweli, hilo hatuwezi kukubaliana nalo. Ndiyo maana nimemwelekeza Kamishna wa Madini wa Kanda, tuangalie namna ya kubadilisha uongozi hapa Mererani ili tuweze kupata mtu ambaye anaweza kusimamia vizuri.”
Aidha, Naibu Waziri aliongeza kuwa, zipo taarifa kuhusu baadhi ya Maafisa wa Wizara waliopangwa kufanya kazi Mererani kutokutimiza wajibu wao ipasavyo kwa kutokuwepo mahali pa kazi kwa muda wote wa kazi kama wanavyopaswa, badala yake wanakuwepo kwa muda mfupi na kuondoka.
“Hili jambo haliwezi kuvumiliwa kwenye Wizara yetu. Kwahiyo, tunataka tudhibitiane na tusimamiane vizuri ili maana halisi ya ndoto ya Rais wetu aliyokuwa nayo katika kudhibiti madini haya iweze kutimia.”
Kwa upande wake, Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini ambaye pia ni Kamishna wa Madini Tanzania, Profesa Shukrani Manya, akisisitiza kuhusu umuhimu wa udhibiti wa utoroshwaji madini, alisema kuwa, dhamira ya Serikali kujenga Ukuta husika ni kuhakikisha changamoto ya kutorosha madini inafika mwisho ili rasilimali hizo zinufaishe Taifa ipasavyo.
“Ziara hii imetufanya tubaini kuwa udhibiti wa utoroshaji madini uliopo unapaswa kuwekewa mkazo kwa kuhakikisha maelekezo ya Serikali yanayotaka kila Idara husika kuweka mbinu zaidi za udhibiti, yanatekelezwa ipasavyo.”
Ukuta unaozunguka migodi ya madini ya Tanzanite Mererani, ulizinduliwa rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, John Pombe Magufuli, Aprili 6 mwaka huu; kufuatia agizo alilolitoa yeye mwenyewe kama njia ya kudhibiti utoroshwaji wa madini hayo adhimu.
Imeandaliwa na:
Veronica Simba, Manyara
Afisa Habari,
Wizara ya Madini,
Kikuyu Avenue,
P.O Box 422,
40474 Dodoma,
Simu: +255-22-2121606/7, Nukushi: +255-22-2121606,
BaruaPepe: info@madini.go.tz,
Tovuti: madini.go.tz
by: madini
Waziri wa Madini, Doto Biteko ameyataka Mabenki ya ndani kushirikiana ili kuweza kuzikopesha kampun…
by: madini on: April 23, 2021, 5:11 a.m.
Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula amesema kuwa katika kipindi cha mwezi Julai, 202…
by: madini on: April 28, 2021, 12:51 p.m.
’Nimeona Nyuso Zenye Furaha , Amani na Utulivu’’ Ninayo furaha kuwa nanyi hapa ili tuanze safari hi…
by: madini on: Jan. 10, 2022, 2:55 p.m.
Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa ameiagiza Tume ya Madini kutafuta Masoko ya wanunuzi wa…
by: madini on: Jan. 30, 2022, 9:32 a.m.