[Latest Updates]: Biteko atoa wito kwa wadau kuzingatia sheria mpya ya madini

Tarehe : March 26, 2018, 8:59 a.m.
left

Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko ametoa wito kwa wadau wote wa sekta ya madini nchini, kuzingatia sheria mpya ya madini ambayo inaelekeza namna bora ya usimamizi wa sekta hiyo.

Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko na Ujumbe aliofuatana nao, wakikagua migodi mbalimbali ya uchimbaji wa madini ya dhahabu na mawe ya nakshi katika vijiji vya Nholi, Itiso na Ntyuka, wakati wa ziara yake ya kazi mkoani Dodoma, Machi 22 mwaka huu.[/caption]

Alitoa wito huo jana, Machi 22 mwaka huu kwa nyakati tofauti, alipokuwa katika ziara ya Mkoa wa Dodoma, kukagua shughuli mbalimbali za madini.

“Moja ya mambo muhimu ambayo sheria mpya ya madini inaelekeza ni kutunza rekodi za uzalishaji wa madini ili Serikali iweze kujua ni kitu gani kinazalishwa na hatimaye tuweze kujua kodi gani zinalipwa na wenye leseni husika,” alifafanua.

Aidha, Naibu Waziri aliwataka wenye leseni kushirikiana na wachimbaji wadogo wa madini ili waweze kunufaika kupitia kazi wanazofanya. “Kwa maneno mengine, asitokee mtu wa kumnyanyasa mchimbaji mdogo eti kwa sababu tu ana leseni,” alisisitiza.

Akizungumza na wamiliki wa leseni pamoja na wachimbaji wadogo wa madini wa dhahabu katika eneo la Nholi wilayani Bahi, Naibu Waziri alipongeza uamuzi wao wa kuanzisha kampeni ifikapo Aprili mwaka huu, kupanda miti kwenye maeneo yao ili kurejesha hali nzuri ya mazingira.

Vilevile, aliwaagiza kuweka wigo kuzunguka mashimo yaliyo wazi ili kuonyesha hali ya tahadhari kuwa eneo hilo ni hatari na linaweza kusababisha ajali, ikiwa ni hatua mojawapo ya kuzingatia usalama migodini.

Akizungumzia changamoto kuu iliyowasilishwa kwake na wachimbaji wa mawe ya nakshi aina ya Granite na Dorelite Dyke katika maeneo ya Itiso wilayani Chamwino na Ntyuka Wilaya ya Dodoma Mjini, kuhusu vibali vya kusafirisha mawe hayo nje ya nchi, Biteko alisema kuwa awali Serikali ilisimamisha utoaji vibali hivyo kuzuia usafirishaji wa mawe ghafi nje ya nchi.

Mashine maalum ikikata jiwe la nakshi aina ya Dorelite Dyke katika Mgodi unaochimba mawe hayo uliopo Itiso wilayani Chamwino Mkoa wa Dodoma. Picha hii ilichukuliwa wakati wa ziara ya Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko mgodini hapo, Machi 22 mwaka huu.[/caption]

“Changamoto iliyokuwepo awali, ni kuwa wako watu walikuwa wanasafirisha madini nje ya nchi yakiwa ghafi, yanaongezwa thamani huko kasha tunarejeshewa sisi tununue bidhaa hizo.”

Akifafanua zaidi, alisema kuwa, jambo linalotia moyo ni kwamba uongezaji thamani madini hivi sasa umeanza kufanyika nchini kwa kiwango kinachotakiwa kusafirishwa nje ya nchi. Alisema, jambo hilo hilo litaleta manufaa kwani thamani, ajira na teknolojia vyote vitabaki ndani na manufaa yatabaki ndani ya nchi pia.

Alipongeza wachimbaji wa mawe ya nakshi wa Itiso na Ntyuka ya kudhamiria kujenga mitambo ya uongezaji thamani mawe hayo katika maeneo husika.

Alisema kiu ya Serikali ni kuona madini yanayochimbwa Tanzania, yanaongezwa thamani nchini na hatimaye kusafirisha bidhaa zinazotokana na madini hayo na kuziuza katika nchi nyingine mbalimbali na siyo vinginevyo.

Aidha, Naibu Waziri aliwasisitiza wamiliki wote wa leseni za madini kufanya kazi zao huku wakizingatia kujenga mahusiano mema na jamii zinazowazunguka.

Alisema kuwa kmujibu wa kanuni mpya iliyopo hivi sasa, mwenye leseni anapaswa kuwasilisha mpango wake wa utoaji huduma kwa jamii (CSR) kwenye Halmashauri husika ili iuthibitishe mpango huo kabla ya utekelezaji wake.

“Ule utaratibu wa mtu anajifungia ofisini, anasema nitawajengea shule pasipo Serikali ya Kijiji au Wilaya kujua, tumeufuta kwa sababu mwanzo ulikuwa unatengeneza matatizo mengi,” alifafanua Biteko.

Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko na Ujumbe aliofuatana nao, wakikagua migodi mbalimbali ya uchimbaji wa madini ya dhahabu na mawe ya nakshi katika vijiji vya Nholi, Itiso na Ntyuka, wakati wa ziara yake ya kazi mkoani Dodoma, Machi 22 mwaka huu.[/caption]

Alisema, Serikali itafanya kazi ya kuangalia na kuthibitisha thamani halisi ya fedha zitakazotumika katika mpango huo, ili kujiridhisha.

Naibu Waziri alimwagiza Afisa Madini Mkazi wa Dodoma Silimu Mtigile kuandaa na kuendesha semina siku ya Jumatatu, Machi  26 mwaka huu, kwa ajili ya wachimbaji wa eneo la Nholi kuhusu sheria mpya ya madini, kufuatia maombi waliyowasilisha kwake alipokuwa akizungumza nao.

Hata hivyo, alisema kuwa semina za aina hiyo zitaendelea kutolewa katika maeneo mbalimbali nchini kote ili kuwajengea uelewa wa sheria hiyo mpya wadau wa madini waweze kufahamu haki na wajibu wao.

Akizungumzia suala la baadhi ya watu kueneza propaganda kuhusu sheria hiyo kuwa ni kandamizi; Biteko aliwataka watanzania kupuuza kauli hizo kwani sheria husika imelenga kuwanufaisha watanzania na siyo kinyume chake.

“Kama kuna bepari anadhani kwamba tunaweza kurudi nyuma katika hili, amekwama. Heri tuwe na wawekezaji wachache wanaofuata sheria kuliko kuwa nao wengi wenye kutaka tu kuchuma mali na kuondoka.”

Katika ziara hiyo, Naibu Waziri Biteko aliambatana na Afisa Madini Mkazi wa Dodoma Silimu Mtigile, wataalam kutoka wizarani na ofisi ya madini Dodoma pamoja na viongozi wa Wilaya na Halmashauri akiwemo Mkuu wa Wilaya ya Bahi Elizabeth Kitundu.

Imeandaliwa na:

Veronica Simba, Dodoma

Afisa Habari,

Wizara ya Madini,

Kikuyu Avenue,

P.O Box 422,

40474 Dodoma,

Simu: +255-22-2121606/7, Nukushi: +255-22-2121606,

BaruaPepe: info@madini.go.tz,                                             

Tovuti: madini.go.tz

by: madini

Latest News
Biteko atoa wito Mabenki ya ndani kuungana kukope…

Waziri wa Madini, Doto Biteko ameyataka Mabenki ya ndani kushirikiana ili kuweza kuzikopesha kampun…

by: madini on: April 23, 2021, 5:11 a.m.

Ukusanyaji wa Maduhuli Sekta ya Madini Wafikia As…

Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula amesema kuwa katika kipindi cha mwezi Julai, 202…

by: madini on: April 28, 2021, 12:51 p.m.

Aliyoyasema Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Adol…

’Nimeona Nyuso Zenye Furaha , Amani na Utulivu’’ Ninayo furaha kuwa nanyi hapa ili tuanze safari hi…

by: madini on: Jan. 10, 2022, 2:55 p.m.

Tume ya Madini Yaagizwa Kutafuta Masoko

Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa ameiagiza Tume ya Madini kutafuta Masoko ya wanunuzi wa…

by: madini on: Jan. 30, 2022, 9:32 a.m.

Read News
Contact Us
Permanent Secretary,
Ministry of Minerals,
Madini Street,
Government City, Mtumba
P. O. Box 422,
Dodoma, Tanzania
Email: ps@madini.go.tz
Copyright©2021 Ministry of Minerals