Tarehe : Nov. 4, 2018, 7:05 a.m.
Serikali imesema inapitia upya Leseni zote za Utafiti wa Madini kwenye Wilaya ya Nyang’hwale Mkoani Geita ili kubaini ambazo hazijaendelezwa ili zifutwe na maeneo hayo kutengwa kwa ajili ya kuwapatia wachimbaji wadogo.
Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko akiwapungia mkono wachimbaji wadogo wa Bululu (hawapo pichani) mara baada ya kuwasili kijijini hapo kwa ajili ya kuzungumza nao. Kulia kwake ni Mbunge wa Jimbo la Nyang’hwale, Hussein Amar.[/caption]
Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko amebainisha hayo hivi karibuni wakati wa mkutano na wachimbaji wadogo wa Kijiji cha Bululu, Kata ya Nyamtukuza wilayani humo.
Akizungumza kwa niaba ya wachimbaji hao, Mbunge wa Jimbo la Nyang’hwale, Hussein Amar alisema wananchi wa wilaya hiyo wanateseka kwa kukosa maeneo ya kuchimba madini na kwamba wamekuwa wakikimbizwa kwenye maeneo waliyokuwa wakifanya uchimbaji kwa madai kuwa maeneo hayo yanamwenyewe.
Akijibu maombi hayo, Biteko alisema Rais John Magufuli anataka kuona Watanzania wanyonge wananufaika na rasilimali zao ikiwemo rasilimali madini.
“Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Dkt John Pombe Magufuli ni Serikali inayowaangalia wanyonge. Haitaki Watanzania wanyonge waendelee kuteseka na kunyanyaswa. Muda umefika Watanzania nao wanufaike,” alisema Biteko.
Alifafanua kuwa Sheria ya Madini iliyokuwa ikitumika hapo awali kabla ya Marekebisho ya Mwaka 2017, haikumpa haki Mtanzania lakini hivi sasa inatamka bayana kwamba rasilimali zote ikiwemo madini ni mali ya Watanzania
Mara baada ya kufafanua hayo, Biteko alibainisha kuwa kwenye Mkoa wa Geita kila wilaya yapo maeneo kadhaa yametengwa kwa ajili ya wachimbaji wadogo isipokuwa kwa Wilaya ya Nyang’wale kwakuwa maeneo mengi wilayani humo tayari yana leseni.
Naibu Waziri wa madini, Doto Biteko akizungumza na wachimbaji wadogo wa Bululu (hawapo pichani).[/caption]
Hata hivyo alifafanua kuwa leseni za maeneo wanayohitaji wachimbaji hao zitamaliza muda wake siku chache zijazo “Maeneo mnayohitaji yana leseni; zipo za utafiti na zingine za uchimbaji lakini habari njema ni kwamba zote zinamaliza muda wake,” alisema.
Aliwataka wachimbaji hao kufanya subira kwani maeneo wanayohitaji leseni zilizopo zinamaliza muda wake Machi 30 Mwaka huu na ndipo mpango wa kugawa maeneo hayo utakapofanyika.
Akielezea utaratibu utakaotumika kwenye ugawaji wa maeneo hayo, Biteko aliwataka wachimbaji hao waingie kwenye mfumo rasmi wa kuunda vikundi na wawasilishe orodha ya vikundi hivyo kwa Mkuu wa Wilaya na Ofisi ya Madini ili kuanza mara moja mpango na utaratibu wa ugawaji wa maeneo husika.
“Ugawaji wa maeneo utazingatia vikundi na sio mtu mmoja mmoja ili iwe rahisi pia kupatiwa msaada na Serikali. Kama hamna vikundi undeni sasa na muwasilishe orodha ili taratibu za ugawaji zifanyike,” alisema.
Vilevile aliwakumbusha wajibu wao wa kufuata maelekezo ya Serikali na kulipa kodi sambamba na kuacha tabia ya kutorosha madini. “Ni ushamba kutorosha madini, mtu mjanja ni yule anaelipa kodi ili Serikali ipate fedha ya kuwahudumia wananchi mkiwemo na nyinyi wachimbaji wadogo,” alisema.
Aidha, Naibu Waziri Biteko aliweka bayana kwamba maeneo ambayo hayaendelezwi na hakuna taarifa yoyote iliyowasilishwa kwenye Ofisi za Madini, leseni kwenye maeneo hayo zitafutwa mara moja na maeneo hayo kupatiwa wenye nia ya dhati ya kuyaendeleza.
Imeandaliwa na:
Mohamed Saif,
Afisa Habari,
Wizara ya Madini,
5 Barabara ya Samora Machel,
S.L.P 2000,
11474 Dar es Salaam,
Simu: +255-22-2121606/7, Nukushi: +255-22-2121606,
Barua Pepe: info@madini.go.tz,
Tovuti: madini.go.tz
by: madini
Waziri wa Madini, Doto Biteko ameyataka Mabenki ya ndani kushirikiana ili kuweza kuzikopesha kampun…
by: madini on: April 23, 2021, 5:11 a.m.
Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula amesema kuwa katika kipindi cha mwezi Julai, 202…
by: madini on: April 28, 2021, 12:51 p.m.
’Nimeona Nyuso Zenye Furaha , Amani na Utulivu’’ Ninayo furaha kuwa nanyi hapa ili tuanze safari hi…
by: madini on: Jan. 10, 2022, 2:55 p.m.
Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa ameiagiza Tume ya Madini kutafuta Masoko ya wanunuzi wa…
by: madini on: Jan. 30, 2022, 9:32 a.m.